Ijumaa, 15 Machi 2013

HAYA KWELI NI YA AIBU

UWOYA, NDIKU USO KWA USO RWANDA

Na Mwandishi Wetu
ZIARA ya mastaa wanne wa Bongo Movies nchini Rwanda hivi karibuni, imewakutanisha uso kwa uso wanandoa waliotengana, Irene Pancaras Uwoya na msakata kabumbu, Hamad Ndikumana ‘Kataut’ Ijumaa limebaini.
Irene Pancaras Uwoya akiwa na mumewe Hamad Ndikumana ‘Kataut’ enzi za penzi lao.
Uwoya na Kataut walikutana jijini Kigali baada ya mastaa hao kupata mwaliko wa kiserikali kuhudhuria tuzo za filamu zilizoandaliwa kwa ajili ya wasanii wa Kinyarwanda (Rwanda Movies  Awards).
Chanzo chetu kimesema kwamba, wawili hao ambao walifunga ndoa mwaka 2009 jijini Dar na kubahatika kupata mtoto mmoja aitwaye Dagrei Krish, waliongea kwa muda mrefu na kutoonesha tofauti yoyote.
“Hawakuonesha tofauti yoyote, waliongea vizuri, walikula pamoja na kulala hoteli moja,” kimesema chanzo hicho.
Ndoa ya Uwoya na Kataut ilivunjika  mwanzoni mwa mwaka jana kisha ‘shemeji’ yetu huyo kuondoka Dar kurudi Rwanda kuendesha maisha yake ya kusakata kabumbu katika Klabu ya Rayon.
Hata hivyo, Ndikumana amekuwa akikanusha kuvunjika kwa ndoa hiyo kwa kusema kwamba hakuna kati yake na Uwoya aliyekiri hadharani kwamba ndoa yao imevunjika.
Mastaa wengine walioambatana na Uwoya nchini Rwanda ni pamoja na Vincent Kigosi ‘Ray’, Jacob Steven ‘JB’ na Amri Athuman ‘King Majuto’ ambao wote pamoja na Uwoya walirudi nchini Jumanne iliyopita.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni